Top ad

Top ad

 

WAVAMIZI ENEO LA KIWANDA CHA KUCHAKATA TAKA MABWEPANDE WATAKIWA KUONDOKA MARA MOJA

Posted On: December 14th, 2020

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar Es salaam Mhe.Abubakar Kunenge leo alipofanya ziara ya ukaguzi wa kiwanda cha kuchakata taka kilichopo Kata ya Mabwepande Manispaa ya Kinondoni.

Amesema eneo hilo enye ekari 14,  lilitengwa kwa ajili ya shughuli za uchakataji wa taka ikiwa ni hatua za Serikali za kuhakikisha inatatua kero za uchafu zinazowakabili wananchi katika maeneo yao, lakini pia ni moja ya kitega uchumi kwa kuzalisha mbolea isiyo na kemikali itakayoweza kuuzwa kwa wanachi na wadau mabilimbali na si kwa ajili ya makazi.

 Katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Dar Es Salaam Mhe. Abubakar Kunenge na kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe. Daniel Chongolo wakikagua mradi.

"Ninaagiza wale  wote waliovamia eneo hilo kuondoka mara moja ili kuepukana na adha ya kubomolewa na kuharibiwa mali zao na  ninyi Manispaa wekeni mipaka katika eneo hili ili ijulikane mwanzo na mwisho wake.  Nilazima wana Dar es salaam mjifunze kufuata Sheria, kuitii Sheria na si vinginevyo." Ameagiza RC Kunenge.

Katikati ni Meya wa Manispaa ya Kinondoni Mhe. Songoro Mnyonge

Naye Mstahiki Meya wa Manispaa hiyo Mhe.Songoro Mnyonge alipokuwa akitoa ufafanuzi amesema  kiwanda hiki kinachojengwa kwa ufadhili  kutoka jiji la Humburg Nchini Ujeruman, kinauwezo wa kuchukua tani 50 za taka kwa siku na kuzichakata hadi kufika tani 30 kwa siku moja kwa kutumia mitambo ya kisasa itakayofungwa katika eneo hilo.


Amesema mitambo ya kuchakata taka tayari imefika bandarini ikisubiri ukamilishwaji wa taratibu za kiserikali ili iweze kufungwa tayari kwa kuanza kazi.

Akitoa ufafanuzi wa kiwanda hicho, Afisa Usafishaji wa Manispaa hiyo  Ndg Alban Mugyabuso amesema mfumo mzima wa uchakataji taka hadi kukamilika kwake unatumia siku 14, na kwamba tayari masoko yameshaanza kutafutwa kwajili ya ununuzi wa mbolea isiyo na kemikali itakayopatikana baada ya uchakataji.


Aidha ameeleza kuwa takataka zinazochukuliwa kwa ajili ya uchakataji ni zile zinazotoka masokoni zenye kuoza kwa haraka na siyo chupa za maji wala mifuko ya plastiki.

Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa amewataka TRA na Bandari kushughulikia kwa haraka mitambo hiyo iliyoko bandarini  iweze kutoka ili ifungwe na kiwanda kiweze kufanya kazi.

Imeandaliwa na

Kitengo Cha Uhusiano na Habari.

Manispaa ya Kinondoni.

0 comments:

Post a Comment

 
Top