Top ad

Top ad

KINONDONI YAPONGEZWA KWA UTEKELEZAJI WA ILANI YA UCHAGUZI YA CCM 2015-2020, KWA VITENDO

Posted On: June 19th, 2020

Pongezi hizo zimetolewa na Kamati ya siasa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Kinondoni kwenye kikao cha majumuisho baada ya ziara ya siku mbili ya ukaguzi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Akizitoa pongezi hizo,  Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya kinondoni Ndg Arold Maruma amesema Kinondoni imeonesha uzalendo katika kuhakikisha ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015 hadi 2020, inatekelezwa kwa vitendo kwa kutumia makusanyo yao ya Ndani, Fedha kutoka Serikli kuu pamoja na Fedha kutoka kwa wadau wa maendeleo.

 "Kinondoni kwakweli mmeitendea haki ilani ya uchaguzi ya CCM kwa mwaka 2015-2020, miradi mliotekeleza hapa ni mfano wa kuigwa na mmeacha taswira inayoonekana kwa Wananchi." Ameongeza Mwenyekiti.

Aidha amebainisha kuwa thamani halisi ya fedha imeonekana Katika miradi hiyo kwani mbali na kutumia fedha za ndani, Serikali kuu na wadau, lakini pia  kiasi kilichotumika katika ukamilishaji wake vinaenda sambamba na ubora .

Awali akikabidhi ripoti ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo  kwa Mwenyekiti wa CCM, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe. Daniel Chongolo amesema Kinondoni imeweza kufanikiwa kukamilisha miradi hiyo kutokana na ushirikiano mzuri uliopo baina ya ofisi yake, Ofisi ya Mkurugenzi na Mstahiki Meya.

Ameongeza kuwa viongozi hawa wa Manispaa na  timu zao wamekuwa  na lengo moja la kuiletea Halmashauri hii maendeleo kwa kuwapatia na kusimamia vyema miradi ambayo inakwenda kumaliza changamoto mbalimbali za Wananchi.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Ndugu Aron Kagurumjuli amesema kuwa Halmashauri imekuwa na utaratibu wa kutenga asilimia 60 ya mapato yake ya ndani na  kuipeleka kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo na asilimia 40 inayobaki kutumika katika matumizi mengine ya kuendesha Halmashauri.

Miradi iliyotembelewa na kamati hiyo ni pamoja na ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri,  Ujenzi wa soko la kisasa la magomeni, Ujenzi wa kituo Cha afya Cha kigogo, Ujenzi wa barabara ya akachube, Ujenzi wa zahanati ya Magomeni, zahanati ya Makumbusho , Ujenzi wa uwanja wa mpira wa kisasa uliopo mwenge na Ujenzi wa stendi ya kisasa ya daladala.

Mingine ni ujenzi wa Kiwanda Cha kuchakata taka na kutengeneza mbolea mboji kilichopo mabwepande,  Ujenzi wa Hospitali ya Wilaya iliyopo Mabwepande,  Shule ya sekondari ya wasichana ya kidato Cha tano na sita Mabwe Tumaini girls,  Upanuzi wa kituo cha afya Bunju  na Ujenzi wa shule ya Msingi Mkoani.

Imeandaliwa na

Kitengo Cha habari na Uhusiano

Manispaa ya kinondoni.

0 comments:

Post a Comment

 
Top