Top ad

Top ad

 

JENGENI UTARATIBU WA KUPIMA AFYA ILI KUJUA HATUA ZA KUCHUKUA KATIKA KUJILINDA

Posted On: May 30th, 2021

Rai hiyo imetolewa na Mbunge wa Jimbo la Kinondoni Mhe Abas Tarimba alipokuwa akifunga mafunzo ya siku tatu yaliyofanyika katika Ukumbi wa mikutano wa Manispaa  kwa kamati ya kudhibiti maambukizi ya Virusi vya UKIMWI yenye lengo la kuwajengea uwezo katika kutekeleza majukumu yao.

Amesisitiza kuwa kujua Afya ndio msingi mzima wa mstakabali utakaokutaka  kuchukua hatua stahiki pindi inapotakiwa kufanya hivyo hasa ikizingatiwa takwimu kutoka mwezeshaji wa TACAIDS zinaonesha kutokuwepo na mwamko wa Jamii kuchukua hatua za Afya hali inayoashiria hatari katika ongezeko la maambukizi ya VVU.

Amesema "bado baadhi ya watu hawana mwamko wa kujua afya zao, hali hii inapelekea watu waliokwishapata maambukizi ya VVU  kuishi bila kufuata utaratibu wa kiafya anaotakiwa kuufuata kulingana na maelekezo ya wataalamu na hivyo kusababisha athari kubwa zaidi"

Aidha Amebainisha kuwa Katika kipindi hiki cha mlipuko wa corona, tahadhari kubwa inaelekezwa jinsi ya kupambana na Corona huku watu wakijisahau kuhusu uwepo wa UKIMWI kwenye Jamii.

"UKIMWI upo na tunaishi nao, kila mtu azungumze na nafsi yake ili asifanye yale ambayo  yanapelekea kusambaa kwa maambukizi ya UKIMWI" Ameongeza Mhe Tarimba

Katika hatua nyingine ameshauri kuwa elimu zaidi itolewe kwa wale ambao wameshabainika kuwa na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI ili waweze kuishi wakifuata ushauri wa wataalamu wa afya na kuendelea na shughuli zao za uzalishaji mali.

Imeandaliwa na

Kitengo cha Habari na Uhusiano

Manispaa ya Kinondoni.

0 comments:

Post a Comment

 
Top