Top ad

Top ad

DC CHONGOLO AWAFUNDA VIJANA WAJASIRIAMALI WA BIDHAA ZA NGOZI KUCHANGAMKIA FURSA ZA MIKOPO YA HALMASHAURI

Posted On: November 14th, 2019
Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe. Daniel Chongolo amewataka vijana kutumia fursa inayotolewa na serikali kupitia halmashauri kupata mikopo isiyokuwa na riba ili waweze kujikwamua kiuchumi.
Mhe. Chongolo alitoa kauli hiyo jana wakati akifungua mafunzo kwa vijana wajasiriamali wanaotengeneza bidhaa za ngozi waliopo katika Manispaa ya Kinondoni ambapo miongoni mwao walipata fursa ya kushiriki maonesho ya wakulima nanenane.
Mhe. Chongolo alisema kuwa Manispaa ya Kinondoni inafungu la bajeti kwa ajili ya kutoa mikopo kwa Vijana, wakina mama na watu wenye ulemavu kwa lengo la kuwasaidia kujikwamua katika umasikini hivyo vijana wanapaswa kutumia nafasi hizo wanazozipata kwani itawawezesha kukuza mitaji yao na hivyo kufikia lengo la kuwa na viwanda huku akitolea mfano wa mfanyabiashara mkubwa Marehemu Dk. Reginal Mengi ambaye alifanikiwa kuwa na viwanda kupitia ujasiriamali.
Alifafanua kuwa iwapo watatumia vizuri mafunzo hayo yataleta tija katika kukuza uchumi wa ndani na kwamba serikali kupitia halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni itasimamia kupata mikopo hiyo na hivyo kuwawezesha kupata mashine pamoja na eneo la kujenga kiwanda chakutengeneza bidhaa za ngozi.
“ Nawapongeza sana idara husika ambayo imeandaa haya mafunzo sambamba na maonyesho ya bidhaa za ngozi, vijana mliopo hapa ,tumieni hii fursa mliyoipata, hakuna mafanikio ya siku moja, wote waliofanikiwa walianza kama nyie hapa” alisema Mhe. Chongolo.
“ Tunahitaji watu ambao watakuwa na nia ya kweli ya kujikwamua kiuchumi, inawezekana kuzalisha bidhaa za ngozi kwakuwa Tanzania tunaongoza kwakuwa na mifugo, ukiangalia Dar es Salaam ndio inaongoza kwa kula nyama,kwahiyo tunazana za kutengenezea bidhaa zetu” alifafanua.
Kwaupande wake , Meneja ukuzaji Bidhaa kutoka Tan Tredi , Masha Husein alisema kuwa wataendelea kushirikiana na manispaa ya Kinondoni katika kuwaelimisha wajasiriamali namna ya kufanya biashara kwenye maonesho kwani hiyo imekuwa ni changamoto kubwa kwao.
Alifafanua kuwa, wajasiriamali wengi hawana uelewa wa kutosha kuhusiana na namna ya kushiriki kwenye maonesho mbalimbali wanapopata nafasi jambo ambalo kama Tan Tredi imeliona na hivyo kusisitiza kuwa watahakikisha wanatoa elimu hiyo ili waweze kunufaika.
Naye Mkuu wa Idara ya Mifugo na Uvuvi Dk. Patricia Henjewele alimpongeza Mhe. Chongolo kwakujali vijana na kusema kuwa katika maonesho ya nane nane waliona umuhimu wakukutana na wajasiriamali hao na hivyo kuandaa semina hiyo iliyoambatana na maonesho.
Aidha aliwapongeza Tan Tredi kwakuwezesha maonesho hayo na hivyo kuahidi kuendeleza ushirikiano zaidi katika kutoa elimu kwa wajasiriamali hao.

Imetolewa na
Kitengo cha Habari na Uhusiano
Manispaa ya Kinondoni.

0 comments:

Post a Comment

 
Top