Top ad

Top ad

KINONDONI YASOGEZA HUDUMA KWA WANANCHI, KWA KUFUNGUA VITUO VYA KUKUSANYA MAPATO KATIKA KATA TANO.

Posted On: September 19th, 2018
Hayo yamebainishwa na Mstahiki Meya wa Manispaa hiyo Mh Benjamini Sitta, alipokuwa akiongea na waandishi wa habari katika mahojiano yaliyofanyika mara baada ya kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa Manispaa.
Amesema lengo la ufunguzi wa vituo hivyo  ni kutekeleza mpango mkakati wa kuongeza mapato, unaoenda sambamba na ukusanyaji wake, ikihusisha ulipaji wa tozo mbalimbali katika Halmashauri,  lakini pia ni katika kuwajali wananchi kwa kuwasogezea huduma hiyo kwa ukaribu zaidi kutakakorahisisha ulipaji wa tozo na kodi mbalimbali ambapo hapo awali iliwalazimu kufuata huduma hiyo katika ofisi za Halmashauri.
"leo tulikuwa na kikao cha kawaida cha baraza la madiwani, na katika kikao hicho,  yamejadiliwa mambo mengi yakiwemo mpango mkakati wa kukabiliana na changamoto ya ukusanyaji mapato, ila kama Halmashauri tumekuja na mkakati thabiti wa kukabiliana na swala hilo kwa kufungua vituo vya kimapato katika Kata tano za Halmashauri yetu." Amefafanua Meya Sitta.
Aidha amezitaja Kata na  vituo  hivyo kuwa ni  Bunju, Tegeta-Kibo Complex, Mwenge, Msasani na Mikocheni,na kuanisha huduma zitakazopatikana kuwa ni ukataji na ulipaji wa  leseni za vileo, Ada za kupima afya, ada za TFDA, na ada za SUMATRA kwa vyombo vya usafiri kama vile pikipiki, na Bajaji.
Aidha katika kikao hicho cha Baraza kilichojumuisha wakuu wa idara na vitengo, Wah. Madiwani, Tarura,TAKUKURU, na Jeshi la Polisi, kimejadili ajenda kuu tatu ambazo ni taarifa za utekelezaji wa Kamati mbalimbali za kudumu robo ya nne, taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, pamoja na kuthibitisha taarifa za kamati mbalimbali za kudumu.
Katika hatua nyingine Meya Sitta amewataka wananchi wa Manispaa ya kinondoni kuvitumia vituo vilivyofunguliwa katika Kata na maeneo wanakoishi kwa ajili ya kulipia tozo mbalimbali  kwani ndio njia rahisi ya kuepukana na mlolongo wa foleni wakati wa kupatiwa huduma hizo.
Aidha kikao hicho kimeenda sambamba na kuapishwa kwa Mbunge wa jimbo la Kinondoni Mhe. Abdallah Mtulia, aliyeshinda uchaguzi mara baada ya kufanyika uchaguzi wa  marudio katika jimbo hilo.

Imeandaliwa na
Kitengo cha Uhusiano na Habari.
Manispaa ya Kinondoni.

0 comments:

Post a Comment

 
Top