Top ad

Top ad

KINONDONI YAKABIDHIWA KISIMA CHA MAJI CHENYE THAMANI YA TSH MILIONI KUMI NA NNE ZA KITANZANIA

Posted On: August 31st, 2018
Kisima hicho kilichojengwa kwa ufadhili wa Asasi ya Kiraia ya TIME TO HELP, chenye ukubwa wa mita 104, kimekabidhiwa leo kwa Shule ya Sekondari Boko na Shule ya msingi Boko National Housing zilizopo Kata ya Bunju, Mtaa wa Dovya Manispaa ya Kinondoni.
Akipokea kisima hicho kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Katibu tawala wa Wilaya hiyo,  Bi.Stella Msofe amesema,  ujenzi wa kisima hicho ni kielelezo tosha cha Asasi ya Kiraia ya Time to help kinachoonesha  dhamira ya dhati  ya kuunga mkono jitihada za   Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania chini Rais Dr.John Pombe Joseph Magufuli, ya   kuboresha  miundombinu ya elimu na maji Mashuleni.
"Tunaishukuru sana TIME TO HELP, mlichokifanya mmerudisha nuru kwenye nyuso zilizofubaa, mmedhihirisha uzalendo mlionao kwa Taifa hili, lakini pia mmerudisha uhai kwa wanafunzi hawa kwa kutujengea kisima cha ukubwa wa mita 104, kitakachoziwezesha shule hizi mbili kupata maji."Amesema Katibu Tawala.
Aidha Bi.Msofe amewataka waalimu na wanafunzi wa shule hizo mbili kuhakikisha wanakitunza, wanakilinda, na kukithamini kisima hicho kwa matumizi yaliyokusudiwa.
Akisoma taarifa ya shule kwa mgeni rasmi,  Mkuu wa Shule ya Sekondari Boko  Bi Rosalia Chelesi amesema, Shule inajumla ya wanafunzi 1,015, kati yake wavulana ni 510, na wasichana ni 240, na  kwa upande wa  Shule ya Msingi Boko National Housing idadi ya wanafunzi ni 498, ambapo wavulana ni 258, na wasichana ni 240.
Bi.Chelesi pia ameainisha changamoto zilizopo shuleni hapo kuwa ni ubovu wa madarasa, upungufu wa madawati, ukosefu wa uzio, upungufu wa matundu ya vyoo, uharibifu wa barabara hasa kipindi cha mvua, upungufu wa nyumba za waalimu, pamoja na ukosefu wa umeme kwa shule ya Msingi Boko National Housing.
Imeandaliwa na
Kitengo cha Uhusiano na habari.
Manispaa ya Kinondoni.

0 comments:

Post a Comment

 
Top