Top ad

Top ad

WITO WATOLEWA KWA ASASI ZA KIRAIA KUSHIRIKI KAMPENI YA UBORESHAJI MIUNDOMBINU YA ELIMU KINONDONI

Posted On: January 30th, 2019
Wito huo umetolewa leo na Afisa maendeleo ya jamii Manispaa hiyo Bi Halima Kahema, alipokuwa akifungua mkutano wa siku moja uliowakutanisha wadau wa maendeleo, maafisa maendeleo ya jamii wa Kata pamoja na Taasisi zisizo za kiserikali zinazofanya shughuli zake katika Manispaa hiyo, kwa lengo la kujadili mstakabali mzima wa maboresho ya miundombinu ya Elimu na utatuzi wa changamoto zilizopo katika sekta hiyo.
Amesema katika kumuunga mkono Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye swala zima la elimu, Asasi za Kiraia na Taasisi zisizo za kiserikali ni vema kuwa na mchango wake wa hiari katika hili.
"Elimu ni yetu sote, hivyo ninyi Asasi za kiraia mliopo Kinondoni, tukishirikiana kwa pamoja kuongeza nguvu katika hili, hakika tutakuwa tumetatua Changamoto kubwa sana katika sekta hii nyeti, ambayo Rais wetu wa awamu ya tano ameipa kipaumbele cha kutosha" Amesisitiza Bi.Kahema.
Awali  akifafanua changamoto ya upungufu wa vyumba vya madarasa katika Halmasahuri hiyo,  Afisa Elimu taaluma  Bw Japhet Moshi amesema, upungufu wa vyumba vya madarasa kwa shule za sekondari pekee ni 103, kwani  idadi ya wanafunzi waliomaliza kidato cha nne mwaka jana ni 4,054,  na waliochaguliwa kujiunga  kidato cha kwanza mwaka huu ni 11,562.
 Amezitaja changamoto nyingine kuwa ni uhaba wa mabweni, matundu ya vyoo vya wanafunzi, nyumba za walimu, huduma ya maji na chakula mashuleni, mazingira, watoto yatima, watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu na huduma za afya.
Naye Balozi wa Uturuki nchini Tanzania Bw Mohammed Yusuph, alipotakiwa kuzungumza aliahidi kushirikiana na Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuhakikisha maswala ya miundombinu ya elimu, pamoja na watoto waishio katika mazingira hatarishi yanapatiwa suluhisho kwa kiasi cha kuridhisha, ili miundombinu ya elimu iweze kuboreshwa.
Mkutano huo uliofanyika katika ukumbi wa shule ya Msingi Oysterbay umekutanisha Asasi za Kiraia zaidi ya 400, kwa lengo la kuelezea na kuainisha mpango wa Halmashauri wa kujenga vyumba 100 vya madarasa ili kupambana na changamoto hiyo ambayo ndio kikwazo kikubwa katika sekta hii.
Imeandaliwa na
Kitengo Cha Habari na uhusiano
Manispaa ya Kinondoni.

0 comments:

Post a Comment

 
Top